Breaking News

MWANAFUNZI CHUO CHA TAIFA CHA USAFIRISHAJI (NIT) AHUKUMIWA JELA MIEZI 12 AU FAINI MILIONI 5 KWA KUCHAPISHA MAUDHUI MTANDAONI BILA LESENI


Julius Warioba mwenye umri wa miaka 23, ambaye ni mwanafunzi wa mwaka wa pili katika Chuo cha Taifa cha Usafirishaji NIT, amehukumiwa kulipa TZS. milioni 5 au kwenda jela mwaka 1 baada ya kukutwa na hatia ya kuchapisha maudhui mtandaoni bila kuwa na leseni

Warioba ambaye ni mshereheshaji (MC) anadaiwa kuchapisha maudhui kupitia Televisheni ya mtandaoni  inayojulikana kwa jina Mc Warioba, bila kuwa na kibali kutoka TCRA wakati wakijua kuwa ni kinyume cha sheria ya Mtandao.

Mbali na faini, Mahakama  imetaifisha kompyuta aina ya Apple na simu ya mkononi aina ya Iphone ambavyo vilitumika katika kuchapisha maudhui hayo.

Hata hivyo, mshtakiwa huyo amefanikiwa kulipa faini na hivyo kukwepa kifungo.

Hukumu hiyo imetolewa jana  Jumatatu Agosti 26, 2019  na Hakimu Mkazi Mkuu wa Mahakama ya Kisutu, Dar es Salaam , Janeth Mtega baada ya mshtakiwa kutiwa hatiani.