Breaking News

WAZIRI WA ZAMANI, ATAJWA KWENYE KESI YA UHUJUMU UCHUMI

Aliyekuwa Waziri wa Serikali ya awamu ya tatu, Edger Maokola Majogo, ametajwa katika kesi ya uhujumu uchumi inayomkabili mfanyabiashara Mohamed Yusufali na wenzake wawili, kwamba alimdhamini Alhaji Kilahama kukopa Dola za Marekani 500,000 kwa kampuni ya washtakiwa.
Hayo yalidaiwa  jana katika Mahakama Kuu, Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi, wakati shahidi wa kwanza, Dimon Mwakababu, ambaye  ni Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) Wilaya ya Pangani alipokuwa akitoa ushahidi  mbele ya Jaji Lilian Mashaka.
Shahidi alidai Majogo aliyewahi kuwa Waziri wa Nishati na Madini, alimdhamini Alhaj Kilahama aliyechukua mkopo wa Dola 500,000 kutoka Kampuni ya Superial Financing Solution inayomilikiwa na washtakiwa.
Akiongozwa na Wakili wa Serikali Mwandamizi, Christopher Maigwa, alidai mkopo huo uliombwa Novemba 19, mwaka 2014 ambapo fomu ya mkopo huo iliambatanishwa na tathmini ya nyumba ya Majogo iliyopo Msasani Peninsula, yenye thamani ya Sh 1,580,000,000.
Alidai mkopo ulikuwa wa muda wa mwaka mmoja kwa riba ya asilimia 30. Shahidi aliendelea kutolea maelezo fomu nyingine za mikopo ikiwemo ya James Masanja, aliyechukua mkopo wa Sh milioni tatu kwa riba ya asilimia 30.
Alidai katika fomu inaonyesha mkopo uliombwa Agosti 4, mwaka 2014 na moja ya viambatanisho vilivyopo ni fomu ya Kampuni ya Superial Finacing Solution ya makubaliano ya mauzo ya gari aina ya Noah, muuzaji akiwa kampuni hiyo, na mnunuzi akiwa Moshi Kembo na gari iliuzwa.
Kwa mujibu wa Mtanzania digital. Shahidi alidai fomu nyingine ya maombi ya mkopo ya Joha Kilabuka aliyeomba mkopo wa Sh milioni 5.5 kwa mwezi mmoja kwa riba ya asilimia 30 ambapo chini ya fomu  kuna maneno yaliyoandikwa kwa mkono yanayosomeka ‘nimepokea dhahabu katika hali nzuri na salama Septemba 30, mwaka 2013’.

Washtakiwa wengine katika kesi hiyo ni Alloycious Gonzaga na Isaack Kasanga ambao katika kesi hiyo wanakabiliwa na jumla ya mashtaka 45 yaliwemo ya kula njama, kughushi, kuwasilisha nyaraka za uongo, utakatishaji fedha na kuisababishia Serikali hasara ya Sh 2,967,959,554 na dola za  Marekani 12,507.

Usikubali kupitwa na chochote kile tembelea App hii kila mara kupata Habari zote zinazojiri Tanzania na nje ya Tanzania katika Mapenzi na Mahusiano, Elimu, Ajira, Michezo, Maisha, Siasa na Burudani.